2:05 AM
Ukweli wa Ndani wa Kazi ya Kushinda (4)

Kukamilishwa kuna maana gani? kushindwa kuna maana gani? Ni vigezo vipi mtu anapaswa kuwa navyo ili apate kushindwa? Na ni vigezo vipi mtu anapaswa kuwa navyo ili afanywe mkamilifu? Kushinda na kukamilisha yote yanakusudiwa kumfanyia kazi mwanadamu ili aweze kurudi katika asili yake na awe huru na tabia zake potovu za shetani na ushawishi wa Shetani. Huu ushindi huja mapema katika mchakato wa kumfinyanga mwanadamu, ikiwa na maana kwamba ni hatua ya kwanza ya kazi. Kukamilisha ni hatua ya pili, au hitimisho la kazi. Kila mwanadamu ni lazima apitie hali ya kushindwa; la sivyo hataweza kumfahamu Mungu na hawezi kujua kuwa kuna Mungu, yaani, hawezi kumtambua Mungu. Na iwapo mtu hamtambui Mungu, hataweza kufanywa mkamilifu na Mungu kwa sababu hatakuwa na vigezo vya kufanywa mkamilifu. Ikiwa humtambui Mungu, utawezaje kumfahamu? Utawezaje kumtafuta? Aidha, hutaweza kumshuhudia, wala kumtosheleza. Kwa hivyo, kila anayetaka kukamilishwa, hatua ya kwanza lazima iwe kupitia kazi ya kushinda. Hili ndilo sharti la kwanza. Ila, iwe ni kushinda au ukamilifu, kila moja ni lengo la mwanadamu afanyaye kazi na kubadilishwa na kazi hiyo, na kila moja ni kipengele katika kazi ya kusimamia mwanadamu. Hizi hatua mbili ndizo zinahitajika kumgeuza yeyote kuwa mtu mkamilifu; hakuna moja kati yazo inaweza kurukwa. Ni kweli kuwa “kushindwa” hakuonekani kuwa ni jambo zuri, ila ni kweli kuwa mchakato wa kumshinda mtu ni mchakato wa kumbadilisha mwanadamu. Baada ya kushindwa, unaweza kuwa hujapoteza tabia yako mbovu kabisa, ila utakuwa umeijua. Kupitia kazi ya kushinda, utapata kujua uduni wa ubinadamu wako, na vilevile kufahamu utovu wako wa nidhamu. Japo hutaweza kuyaacha haya au kuyabadilisha ndani ya muda mfupi wa kazi ya kushinda, utayajua baadaye. Haya yanaujenga msingi wa ukamilifu wako. Kwa hivyo kushinda na kukamilisha yote yanafanywa kumbadilisha mwanadamu, kumtoa mwanadamu tabia zake mbovu za Kishetani ili ajitolee kikamilifu kwa Mungu. Ni kwamba tu kushindwa ni hatua ya kwanza katika kubadilisha tabia ya mwanadamu na pia hatua ya kwanza ya mwanadamu kujitoa kikamilifu kwa Mungu, hatua iliyo chini ya ukamilifu. Tabia za maisha ya mtu aliyeshindwa hubadilika kiasi kidogo kuliko ya mtu ambaye amepata ukamilifu. Kushindwa na kufanywa mkamilifu ni tofauti kabisa kwa kuwa ni hatua tofauti za kazi na kwa kuwa huhitaji vigezo tofauti kutoka kwa wanadamu, huku ushindi ukiwa na vigezo vya chini na ukamilifu ukiwa na vigezo vya juu. Walio wakamilifu ni wenye haki, watu watakatifu na safi; wao ni udhihirisho wa kazi ya kusimamia wanadamu, au matokeo ya mwisho. Japo si wanadamu wasio na doa, ni watu wanaotaka kuishi maisha ya thamani. Lakini walioshindwa hukiri tu kwa vinywa vyao kuwa Mungu Yupo; wanakiri kuwa Mungu amepata mwili, kwamba neno linaonekana katika mwili, na kwamba Mungu amekuja duniani kufanya kazi ya hukumu na kuadibu watu. Aidha wanakiri kuwa hukumu na kuadibu kwa Mungu na mapigo Yake na usafishaji Wake ni faida kwa mwanadamu. Yaani, wameanza kuwa na sifa za ubinadamu, na wana ufahamu mdogo kuhusu maisha ila si bayana. Kwa maneno mengine, wameanza tu kuwa na ubinadamu. Haya ni matokeo ya kushindwa. Watu waingiapo katika njia ya ukamilifu, tabia zao za zamani zaweza kubadilishwa. Aidha, maisha yao huendelea kukua na taratibu hujitosa zaidi katika ukweli. Wanaweza kuchukia dunia na kuwachukia wale wote ambao hawafuati ukweli. Hususan hujichukia wao wenyewe, na hata zaidi ya hayo, wanajitambua vyema. Wana hiari kuishi kulingana na ukweli na hulenga kufuata ukweli. Hawako radhi kuishi katika mawazo ya bongo zao, na huchukia kujitukuza, kujisifu, na kujiinua kwa mwanadamu. Wananena kwa adabu ya hali ya juu, wanafanya mambo kwa utambuzi na hekima, ni waaminifu na watiifu kwa Mungu. Wakipitia kuadibu na hukumu, wao hawakuwi wanyonge au wasioonyesha hisia tu, bali hutoa shukrani kwa ajili ya kuadibu na hukumu zitokazo kwa Mungu. Wanaamini hawawezi kuishi bila kuadibu na hukumu ya Mungu; wanaweza kupata ulinzi Wake kupitia haya. Hawafuati imani ya amani na furaha na ya kutafuta mkate wa kuwashibisha. Wala hawafuati raha za muda za kimwili. Hili ndilo wakamilifu huwa nalo. Baada ya watu kushindwa, wao hukubali kwamba kuna Mungu. Lakini matendo yo yote ambayo huja na kukubali kuweko kwa Mungu, matendo haya ni machache ndani yao. Neno kuonekana katika mwili lina maana gani kwa kweli? Kupata mwili kuna maana gani? Ni nini ambacho Mungu mwenye mwili amefanya? Ni nini lengo na umuhimu wa kazi Yake? Baada ya kupitia kazi Yake nyingi sana, kupitia matendo Yake katika mwili, umepata nini? Ni baada tu ya kufahamu mambo haya yote ndiyo utakuwa mtu aliyeshindwa. Kama wewe utasema tu kwamba unakubali kuwa kuna Mungu, lakini huwachi kile unachopaswa kuwacha na kukosa kuacha raha za mwili ambazo unapaswa kuacha, na badala yake unaendelea kutamani maliwazo ya mwili kama ufanyavyo daima, huwezi kuachilia ubaguzi wowote dhidi ya ndugu, na kuhusu utendaji mwingi rahisi huwezi kulipa stahili yako kutimiza matendo hayo, basi hilo linathibitisha wewe bado hujashindwa. Kwa hiyo, hata kama unaelewa mengi, yote itakuwa bure. Walioshindwa ni watu ambao wametimiza mabadiliko fulani ya mwanzo na kuingia kwa mwanzo. Kupitia hukumu na kuadibu kwa Mungu huwasababisha kuwa na maarifa ya mwanzo ya Mungu na ufahamu wa mwanzo wa ukweli. Hata kama kuhusu ukweli mwingi wa kina, na wa chembechembe zaidi huwezi kuingia kabisa katika uhalisi wake, unaweza kutia katika vitendo ukweli mwingi wa mwanzo katika maisha yako halisi, kama vile unaohusu raha zako za mwili au hali yako binafsi. Yote haya, bila shaka, ni kile kinachotimizwa ndani ya wale wanaopitia kushinda. Mabadiliko fulani katika tabia yanaweza pia kuonekana ndani ya walioshindwa. Kwa mfano, mavazi na unadhifu wao na maisha yao—haya yanaweza kubadilika. Mtazamo wao kuhusu kumwamini Mungu hubadilika, wao hupata uwazi kuhusu chombo cha ukimbizaji wao, na matamanio yao huongezeka. Wakati wa kushindwa, tabia yao ya maisha inaweza pia kubadilika kwa kukubaliana. Sio kwamba wao hawabadiliki kabisa. Ni vile tu mabadiliko yao ni ya juujuu, ya mwanzo, na madogo zaidi kuliko mabadiliko katika tabia na chombo cha ukimbizaji ambayo yangeonekana baada ya mtu kukamilishwa. Kama wakati wa kushindwa, tabia ya mtu haibadiliki kabisa na hapati hata ukweli kidogo, basi mtu wa aina hii huwa tu kipande cha takataka na ni bure kabisa! Watu ambao hawajashindwa hawawezi kukamilishwa! Na kama mtu hutafuta tu kushindwa, hawezi kufanywa kuwa kamili kwa ukamilifu, hata kama tabia yake ilionyesha mabadiliko fulani ya kukubaliana wakati wa kazi ya kushinda. Yeye pia atapoteza ukweli wa mwanzo aliopata. Kuna tofauti kubwa mno kati ya kiasi cha mabadiliko ya tabia ndani ya walioshindwa na waliokamilishwa. Lakini kushindwa ni hatua ya kwanza katika mabadiliko; ni msingi. Kukosa mabadiliko haya ya mwanzo ni thibitisho kwamba mtu kwa kweli hamjui Mungu kabisa kwa sababu ufahamu huu hutoka kwa hukumu, na hukumu hii ni kipengee kikuu katika kazi ya kushinda. Kwa hiyo, kila mtu aliyekamilishwa amepitia kushindwa. Ama sivyo, hangeweza labda kukamilishwa.

Unasema kwamba unatambua Mungu mwenye mwili na unatambua kuwa Neno laonekana katika mwili, na bado unafanya mambo fulani kinyume, na hutendi kulingana na mahitaji Yake, na humwogopi. Je, huku ni kumtambua Mungu? Unatambua Anachokisema ila unakataa kuyaweka katika vitendo hata yale mambo unayoweza kufanya na huzifuati njia zake. Je, huku ni kumtambua? Unamtambua ila mawazo yako ni kujikinga dhidi Yake, kutomcha kamwe. Ikiwa umeona na kuitambua kazi Yake na unafahamu kuwa Yeye ni Mungu, na bado unaendelea kuwa vuguvugu na bado hujabadilika hata kidogo, basi bado hujapata ushindi. Mtu aliyeshindwa hufanya chochote awezacho; anataka kuingia na kuufikia ukweli wa juu hata kama bado hana uwezo. Ni kwamba tu ana mipaka katika yale anayoweza kufanya, yaani, vitendo vyake vimefungiwa na kuwekewa mipaka. Lakini angalau anapaswa kufanya chochote katika uwezo wake. Ukifanya haya mambo, itakuwa ni kwa sababu ya kazi ya kushinda. Hata ukisema, “Kwa sababu Anaweza kunena maneno mengi ambayo mwanadamu hawezi, ikiwa si Mungu, ni nani?” Kuwa na mawazo kama haya hakumaanishi unamtambua Mungu. Ikiwa unamtambua Mungu, unapaswa kuonyesha hilo kupitia kwa matendo yako halisi. Ukiongoza kanisa lakini usiweze kutenda haki, na kutamani pesa na kufuja pesa za kanisa kisiri kwa faida yako—je, huku ni kutambua kuwa kuna Mungu? Mungu ni mwenye Uweza na wa kumcha. Unawezaje kukosa kuogopa kama kweli unatambua kuwa kuna Mungu? Unawezaje kuwa ulifanya kitu cha kuchukiza namna hiyo? Je, huko kunaweza kuitwa kuamini? Je, kweli wamtambua Mungu? Ikiwa unaweza kufanya jambo la kudharauliwa kama hilo, je, huko kweli ni kumtambua Yeye? Je, unamwamini Mungu? Unayemwamini ni Mungu asiye yakini; ndiyo maana huogopi! Wale wote wanaomtambua Mungu kweli na kumfahamu wanamcha na wanaogopa kufanya chochote kinachompinga na chochote kinachoenda kinyume na dhamiri yao; hususan wanaogopa kufanya chochote kinachoenda kinyume na mapenzi ya Mungu. Hili tu ndilo laweza kuwa ni kumtambua Mungu. Utafanya nini wazazi wako wakikuzuia kumwamini Mungu? Utampenda vipi Mungu ikiwa mume wako asiye muumini anakutendea mema? Aidha utampendaje Mungu ikiwa ndugu na dada zako wanakuchukia? Ikiwa unamtambua, basi utatenda ipasavyo na kuishi kwa kudhihirisha uhalisi katika hali hizi zote. Ukikosa kutenda wazi na kusema tu kwamba unatambua uwepo wa Mungu, basi wewe ni msemaji tu! Unasema unamwamini na kumtambua. Je, unamtambua kwa njia gani? Unamwamini kwa njia gani? Je, unamwogopa? Unamcha? Unampenda moyoni mwako? Unapokuwa na huzuni bila yeyote wa kuegemea, unahisi Mungu ni wa kupendwa, halafu baadaye unasahau. Huku si kumpenda au kumwamini Mungu! Je, Mungu anataka mwanadamu apate nini mwishoni? Hali zote Nilizozitaja, kama vile: kufikiri kuwa wewe ni mtu mkubwa, kwamba unaelewa mambo upesi, kuwadhibiti wengine, kuwadharau wengine, kuwahukumu watu kwa misingi ya sura zao, kuwadhulumu watu waaminifu, kutamani pesa za kanisa, na kadhalika—kuondokewa na sehemu ya tabia mbovu za kishetani kama hizo ndiko kunakotakiwa kuonekana ndani yako baada ya wewe kushindwa.

Kazi ya kushinda inayofanywa kwenu nyie ni ya umuhimu mkubwa sana: Kwa upande mmoja, kusudi la hii kazi ni kukikamilisha kikundi cha watu, yaani, kuwakamilisha na kuwa kundi la washindi, kama kundi la kwanza la watu waliofanywa wakamilifu, yaani matunda ya kwanza. Kwa upande wa pili, ni kuruhusu viumbe wa Mungu kufurahia mapenzi ya Mungu, kupokea wokovu mkubwa wa Mungu, na kupokea wokovu kamili wa Mungu, na kumfanya mwanadamu kufurahia si tu huruma na ukarimu wa upendo, ila muhimu zaidi ni kuadibu na hukumu. Tangu uumbaji wa dunia hadi sasa, yote ambayo Mungu amefanya katika kazi Yake ni upendo, bila chuki yoyote kwa mwanadamu. Hata kuadibu na hukumu uliyoiona ni mapenzi pia, upendo wa kweli na wa dhati zaidi; upendo huu huwaongoza wanadamu kwenye njia sahihi ya maisha ya binadamu. Kwa upande wa tatu, ni kushuhudia mbele ya Shetani. Kwa upande wa nne, ni kuweka msingi wa kueneza kazi ya baadaye ya injili. Kazi yote Aliyoifanya ni kumwongoza mwanadamu kwenye njia sahihi ya maisha ya wanadamu, ili kwamba wawe na maisha ya kawaida ya wanadamu, kwani mwanadamu hajui jinsi ya kuishi. Bila uongozi kama huo, utaishi maisha tupu yasiyo na maana wala thamani, na kamwe hutajua jinsi ya kuwa mwanadamu wa kawaida. Huu ndio umuhimu mkuu wa kumshinda mwanadamu. Nyote ni wa ukoo wa Moabu. Kufanya kazi ya kushinda kwenu ni wokovu wenu mkuu. Nyinyi nyote mnaishi mahala pa dhambi na ufisadi; nyinyi nyote ni watu wapotovu na wenye dhambi. Leo hii hamwezi tu kumwona Mungu, ila la muhimu zaidi, mmepokea kuadibu na hukumu, mmepokea wokovu wa kina, yaani, mmepokea upendo mkubwa zaidi wa Mungu. Yote Ayafanyayo ni mapenzi ya dhati kwako; Hana nia mbaya. Anawahukumu kwa sababu ya dhambi zenu, ili kwamba mweze kujichunguza wenyewe na kupokea wokovu mkubwa. Haya yote hufanywa kumfinyanga mwanadamu. Tangu mwanzo hadi mwisho, Mungu amekuwa Akifanya kila Awezalo kumwokoa mwanadamu, na hakika hayuko tayari kuwaangamiza kabisa wanadamu Aliowaumba kwa mikono Yake Mwenyewe. Sasa Amekuja miongoni mwenu kufanya kazi; je, huu si wokovu zaidi? Je, Angalikuchukia, Angaliendelea kufanya kazi ya kiwango hicho cha juu ili kukuongoza wewe Mwenyewe? Ni kwa nini Ateseke hivyo? Mungu hawachukii wala hana nia mbaya juu yenu. Mnapaswa kufahamu kuwa mapenzi ya Mungu ndiyo mapenzi ya kweli zaidi. Anawaokoa kupitia hukumu kwa sababu tu ya uasi wa mwanadamu; la sivyo, hawangepata wokovu. Kwa kuwa hamjui jinsi ya kuishi, na mnaishi katika mahala pa ufisadi na dhambi na ni mapepo wenye ufisadi na uchafu, Hana moyo wa kuwaacha mpotoshwe zaidi; wala Hana moyo wa kutaka kuwaona mkiishi mahala pachafu kama hapa, mkikandamizwa na Shetani apendavyo, Hana moyo wa kuwaacha mtumbukie Kuzimu. Anataka tu kulipata hili kundi lenu na kuwakomboa vilivyo. Hili ndilo kusudi kuu la kufanya kazi ya kushinda miongoni mwenu—ni kwa ajili ya wokovu tu. Iwapo huwezi kuona kuwa kila kitu unachofanyiwa ni mapenzi na wokovu, ukidhani kuwa ni mbinu tu, njia ya kumtesa mwanadamu na kitu kisichoaminika, basi ni bora urudi duniani mwako uendelee kupata mateso na ugumu wa maisha! Ikiwa uko tayari kuwa kwenye mkondo huu na kufurahia hukumu hii na wokovu huu wa ajabu, na kufurahia baraka hizi ambazo haziwezi kupatikana kokote katika ulimwengu wa wanadamu, na kufurahia mapenzi yake, basi baki kuwa mnyenyekevu kwenye mkondo huu kukubali kazi ya kushinda ili uweze kufanywa mkamilifu. Japokuwa kwa sasa unapitia mateso na usafishaji kwa sababu ya hukumu, mateso haya ni ya thamani na ya maana. Japo kuadibu na hukumu ni usafishaji na ufichuzi usio na huruma kwa mwanadamu, uliokusudiwa kuadhibu dhambi zake na kuadhibu mwili wake, kazi hii haijanuiwa kukashifu na kuuzima mwili wake. Ufichuzi mkali wa neno ni kwa kusudi la kukuongoza kwenye njia sahihi. Ninyi wenyewe mmeipitia sana kazi hii na, ni wazi, haijawaongoza kwenye njia mbaya. Yote ni kukuwezesha kuishi kulingana na ubinadamu wa kawaida, yote ni kitu ambacho kinaweza kutimizwa na ubinadamu wa kawaida. Kila hatua ya kazi hufanywa kwa misingi ya mahitaji yako, kulingana na udhaifu wako, kulingana na kimo chako halisi, na hamjatwikwa mzigo msioweza kuubeba. Japo huwezi kuliona hili wazi kwa sasa, na unajihisi Ninakuwa mgumu kwako, japo unadhani kuwa Ninakuadibu na kukuhukumu na kukuadibu kila siku kwa kuwa Ninakuchukia, na ingawa unachokipokea ni kuadibu na hukumu, hali halisi ni kuwa yote ni mapenzi kwako, pia ni ulinzi mkubwa kwako. Ikiwa huwezi kung’amua maana ya ndani ya kazi hii, basi huna njia ya kuendelea katika uzoefu wako. Unapaswa kuliwazwa kwa sababu ya huo wokovu. Usikatae kuzirudia busara zako. Baada ya kusafiri umbali huu, unapaswa kuuona wazi umuhimu wa kazi hii ya kushinda. Hupaswi tena kushikilia mtazamo fulani kama huo!

kutoka katika Neno Laonekana katika Mwili

Chanzo: Kanisa la Mwenyezi Mungu

 

 

Views: 85 | Added by: flickrpinquorettfb | Tags: Matamshi ya Kristo | Rating: 0.0/0
Total comments: 0
avatar