1:21 AM
Kwa nini makanisa yanaweza kupotoka na kuwa dini?
Maneno Husika ya Mungu:
Kwa nini inasemekana kwamba vitendo vya walio katika makanisa ya kidini vimepitwa na wakati? Ni kwa kuwa wanayoyaweka katika vitendo ni tofauti na kazi ya leo. Katika Enzi ya Neema, walichotenda kilikuwa sahihi, ila kwa kuwa enzi yenyewe imepita na kazi ya Mungu kubadilika, vitendo vyao hatua kwa hatua vimepitwa na wakati. Vimeachwa nyuma na kazi mpya na mwangaza mpya. Ikiwa imesimama juu ya msingi wake asili, kazi ya Roho Mtakatifu imepiga hatua kadhaa kwa kina. Na bado watu hao wamebaki katika hatua ya asili ya kazi ya Mungu na bado wanapenyeza katikati ya vitendo na mwangaza wa zamani. Kazi ya Mungu yaweza kubadilika pakubwa kwa miaka mitatu au mitano, hivyo si mabadiliko hata makubwa zaidi yaweza kuja kwa kipindi cha miaka zaidi ya 2000? Ikiwa mwanadamu hana vitendo vipya ama mwangaza mpya, inamaanisha hajaenda sawia na kazi ya Roho Mtakatifu. Hili ni anguko la mwanadamu; uwepo wa kazi mpya ya Mungu hauwezi kukanwa kwa sababu, leo hii, wale walio na kazi asili ya Roho Mtakatifu bado wanashikilia vitendo vilivyopitwa na wakati. Kazi ya Roho Mtakatifu daima inasonga mbele, na wote walio katika mkondo wa Roho Mtakatifu wanafaa waendelee mbele na kubadilika, hatua kwa hatua. Hawapaswi kukwama katika hatua moja. Ni wale tu wasioifahamu kazi ya Roho Mtakatifu ndio wanaweza kubaki katika hatua ya kazi ya Mungu ya awali na wasikubali kazi mpya ya Roho Mtakatifu. Ni wale tu walio waasi ndio watakosa uwezo wa kuipokea kazi ya Roho Mtakatifu. Ikiwa vitendo vya mwanadamu haviendani na mwendo wa kazi mpya ya Roho Mtakatifu, basi vitendo vya mwanadamu hakika vimetengana na kazi ya leo na kwa hakika havilingani na kazi ya leo. Watu waliopitwa na wakati kama hawa hawawezi kutimiza mapenzi ya Mungu, na zaidi hawawezi kuwa wale watu wa mwisho ambao watamshuhudia Mungu. Aidha, kazi nzima ya usimamizi haiwezi kutimilika miongoni mwa kundi la watu kama hao. Kwa wale walioshikilia sheria za Yehova kipindi fulani, na wale walioumia wakati fulani chini ya msalaba, ikiwa hawawezi kukubali hatua ya kazi ya siku za mwisho, basi yale yote waliyofanya ni bure na yasiyofaa. Dhihirisho la wazi zaidi wa kazi ya Roho Mtakatifu ni kwa kuyakumbatia ya sasa, sio kushikilia ya zamani. Wale ambao hawajiendelezi na kazi ya leo, na wale ambao wametengwa na utendaji wa leo, ni wale wanaopinga na hawaikubali kazi ya Roho Mtakatifu. Watu kama hao wanaipinga kazi ya Mungu ya sasa. Ijapokuwa wanashikilia nuru ya zamani, hili halimaanishi kwamba inaweza kukanwa kwamba hawajui kazi ya Roho Mtakatifu. …Walio nje ya mkondo wa Roho Mtakatifu daima hudhani wako sahihi, lakini kwa hakika, kazi ya Mungu ndani yao ilisita zamani na kazi ya Roho Mtakatifu haimo ndani yao. Kazi ya Mungu imeshahamishiwa kwa kundi jingine la watu, kundi ambalo kwalo Anapania kukamilishia kazi Yake mpya. Kwani walio katika dini hawawezi kuikubali kazi mpya ya Mungu, na kushikilia tu kazi kongwe za zamani, hivyo Mungu amewaacha watu hawa na anafanya kazi Yake mpya kwa watu wanaoikubali kazi hii mpya. Hawa ni watu wanaoshiriki katika kazi Yake mpya, na usimamizi Wake utatimilika kwa njia hii tu.
kutoka katika “Kazi ya Mungu na Utendaji wa Mwanadamu” katika Neno Laonekana katika Mwili
Katika kila hatua ya kazi ya Mungu yapo pia matakwa sawia kwa mwanadamu. Wale wote walio katika mkondo wa Roho Mtakatifu wanamilikiwa na uwepo na nidhamu ya Roho Mtakatifu na wasiokuwemo katika mkondo wa Roho Mtakatifu wako chini ya utawala wa Shetani na hawana kazi yoyote ya Roho Mtakatifu. Walio katika mkondo wa Roho Mtakatifu ni wale wanaoikubali kazi mpya ya Mungu, wanaoshiriki katika kazi mpya ya Mungu. Iwapo walio ndani ya mkondo huu hawana uwezo wa kushirikiana, na hawawezi kuweka ukweli unaotakiwa na Mungu katika vitendo wakati huu, basi watafundishwa nidhamu, na hali ikiwa mbaya zaidi kuachwa na Roho Mtakatifu. … Sio hivyo kwa watu wasioikubali kazi mpya: Wako nje ya mkondo wa Roho Mtakatifu, na nidhamu na lawama ya Roho Mtakatifu hayatumiki kwao. Kila siku hawa watu wanaishi ndani ya mwili, wanaishi ndani ya akili zao, na yote wayafanyayo ni kulingana na mafundisho ya kidini yaliyozalishwa na uchanganuzi pamoja na utafiti wa bongo zao. Si matakwa ya kazi mpya ya Roho Mtakatifu sembuse ushirika na Mungu. Wale wasioikubali kazi mpya ya Mungu hawana uwepo wa Mungu na, zaidi, wanakosa baraka na ulinzi wa Mungu. Maneno na matendo yao mengi yanashikilia matakwa ya zamani ya kazi ya Roho Mtakatifu; ni mafundisho ya kidini, si ukweli. Mafundisho na taratibu kama hizo ni thibitisho la kutosha kuwa kitu cha pekee kinachowaleta pamoja ni dini; si watu walioteuliwa au vyombo vya kazi ya Mungu. Mkutano wa wale wote walio miongoni mwao unaweza tu kuitwa mkutano mkubwa wa watu wa dini, na bali hauwezi kuitwa kanisa. Huu ni ukweli usioweza kubadilishwa. Hawana kazi mpya ya Roho Mtakatifu; wakifanyacho kinaonekana chenye kunuka dini, wanachoishi kwa kudhihirisha katika maisha yao kinaonekana kimejaa dini; hawana uwepo na kazi ya Roho Mtakatifu, sembuse kustahiki kupokea nidhamu au nuru ya Roho Mtakatifu. Watu hawa wote ni miili isiyo na uhai, na funza wasio na mambo ya kiroho. Hawana ufahamu wa uasi na pingamizi wa mwanadamu, hawana ufahamu wa uovu wote wa mwanadamu, sembuse kujua kazi yote ya Mungu na mapenzi ya sasa ya Mungu. Wote ni watu wapumbavu, waovu, ni watu duni wasiostahili kuitwa waumini!
kutoka katika “Kazi ya Mungu na Utendaji wa Mwanadamu” katika Neno Laonekana katika Mwili
Watu wakichukulia ukweli kama mfumo wa imani wa kufuatwa, je, wana uelekeo wa kutumbukia katika utaratibu wa dini? Na tofauti kati ya aina hii ya utaratibu wa dini na Ukristo ni gani? Ingawa kile ambacho kinasemekana huenda kikawa cha kina zaidi na cha kusonga mbele zaidi, kikiwa aina fulani ya mafundisho na aina fulani ya utaratibu, basi si kimekuwa Ukristo? Kuna tofauti kati ya mafundisho ya zamani na mapya, lakini ikiwa mafundisho hayo ni aina ya nadharia tu na yakiwa aina ya utaratibu tu, aina ya mafundisho kwa watu—na, vilevile, hawawezi kupata ukweli kutoka kwayo au kuingia katika uhalisi wa ukweli, basi si imani yao ni sawa na Ukristo? Kimsingi, je, si huu ni Ukristo? (Ndiyo.) Kwa hivyo katika tabia yenu na utendaji wa wajibu wenu, ni vitu gani ambavyo kwavyo mna maoni sawa au yanayofanana na wanaoamini katika Ukristo? Ufuatiliaji wa tabia nzuri ya juujuu, kisha kufanya kila uwezalo kujibunia kisingizio kwa kutumia sura ya mambo ya roho; kuiga mtu wa kiroho; kutoa sura ya kuthamini mambo ya kiroho katika kile unachosema, kufanya, na kufichua; kufanya mambo machache ambayo, katika fikra na mawazo ya watu, yanastahili kusifiwa—yote haya ni ufuatiliaji wa mambo ya kiroho kwa njia ya uongo, na ni unafiki. Unasimama juu ukinena maneno na nadharia, ukiwaambia watu wafanye matendo mema, wawe watu wema, na walenge kufuatilia ukweli, lakini katika tabia yako mwenyewe na utendaji wa wajibu wako, hujawahi kutafuta ukweli, hujawahi kutenda kwa mujibu wa kanuni za ukweli, hujawahi kuelewa kile kinachosemwa katika ukweli, mapenzi ya Mungu ni nini, viwango ambavyo Anahitaji kwa mwanadamu ni vipi—hujawahi kuchukulia yoyote haya kwa uzito. Unapokabiliwa na masuala fulani, wewe hutenda kabisa kulingana na mapenzi yako na kumweka Mungu kando. Je, vitendo hivi vya nje na hali za ndani ni kumcha Mungu na kuepukana na uovu? Ikiwa hakuna uhusiano kati ya imani ya watu na ufuatiliaji wao wa ukweli, bila kujali wanamwamini Mungu kwa miaka mingapi, je, watakuwa na uwezo wa kumcha Mungu na kuepukana na uovu kwa kweli? (La.) Na kwa hiyo watu kama hao wanaweza kuitembea njia gani? Je, wao hutumia siku zao wakijiandaa na nini? Je, si ni kwa maneno na nadharia? Je, wao hutumia siku zao wakijiandaa, wakivalia maneno na nadharia, ili kujifanya kama Mafarisayo zaidi, kama watu ambao hudhaniwa kwamba humtumikia Mungu zaidi? Vitendo hivi vyote ni nini? Wanafanya tu mambo kwa namna isiyo ya dhati; wanapeperusha bendera ya imani na kufanya kaida za dini, wakijaribu kumdanganya Mungu ili kufikia lengo lao la kubarikiwa. Hawamwabudu Mungu hata kidogo. Mwishoni, je, si kundi kama hilo la watu litaishia tu kama wale walio ndani ya kanisa ambao hudhaniwa kwamba wanamtumikia Mungu, na ambao hudhaniwa kwamba wanamwamini na kumfuata Mungu?
kutoka katika “Ukiiishi mbele ya Mungu Kila Wakati tu Ndio Unaweza Kuitembea Njia ya Wokovu” katika Kumbukumbu za Maongezi ya Kristo
Jina la Mungu ni gani kwa wale wanaomwamini Yehova? Wako katika kikundi cha dini—Uyahudi. Waligeuka kuwa aina ya kundi la dini. Na Mungu huwafafanuaje wale wanaomwamini Yesu? Wanafafanuliwa kama sehemu ya kundi la dini la Ukristo, siyo? Machoni pa Mungu, Uyahudi na Ukristo ni vikundi vya dini. Kwa nini Mungu anawafafanua hivyo? Miongoni mwa wale wote ambao ni washiriki wa mashirika haya ya dini yaliyofafanuliwa na Mungu, je, kuna wowote wanaomcha Mungu na kuepukana na uovu, kufanya mapenzi ya Mungu, na kufuata njia ya Mungu? (La.) Machoni pa Mungu, je, wale wote ambao humfuata Mungu kwa maneno tu wanaweza kuwa watu Anaowatambua kama waumini katika Mungu? Je, wote wanaweza kuwa na uhusiano na Mungu? Je, wote wanaweza kuwa walengwa wa wokovu wa Mungu? (La.) Ingawa sasa mmekubali kazi ya Mungu ya siku za mwisho, je, siku itakuja ambapo mtashushwa na kuwa kile ambacho Mungu anaona kama kundi la dini? Hiyo inaonekana isiyowazika. Mkikuwa sehemu ya kikundi cha dini machoni pa Mungu, hamtaokolewa na Yeye na inamaanisha ninyi si wa nyumba ya Mungu. Kwa hivyo jaribu kufupisha: Watu hawa ambao wanamwamini Mungu wa kweli kwa maneno tu lakini ambao Mungu anawaamini wao kuwa sehemu ya kikundi cha dini—wanaitembea njia gani? Je, inaweza kusemekana kwamba watu hawa wanaitembea njia ya kupeperusha bendera ya imani bila kamwe kufuata njia Yake au kumwabudu, na badala yake kumtelekeza Mungu? Yaani, wanaitembea njia ya kumwamini Mungu lakini wanamwabudu Shetani, wakitekeleza usimamizi wao wenyewe, na kujaribu kuanzisha ufalme wao wenyewe—je, hiki ni kiini cha hilo? Je, watu kama hawa wana uhusiano wowote na mpango wa Mungu wa usimamizi kwa ajili ya wokovu wa mwanadamu? (La.) Bila kujali ni watu wangapi wanamwamini Mungu, mara tu imani zao zinapofafanuliwa na Mungu kama dini au kikundi, basi Mungu ameamua kuwa hawawezi kuokolewa. Kwa nini nasema hivi? Katika kundi au umati wa watu ambao hawana kazi na mwongozo wa Mungu na ambao hawamwabudu hata kidogo, wanamwabudu nani? Wanamfuata nani? Katika mioyo yao wanamtambua Mungu, lakini kwa kweli, wao huathiriwa na utawala wa hila na udhibiti wa binadamu. Kwa jina, labda wanamfuata mtu fulani, lakini kimsingi, wanamfuata Shetani, ibilisi; wanafuata nguvu ambazo zina uhasama kwa Mungu, ambazo ni maadui wa Mungu. Je, Mungu anaweza kuokoa kundi kama hili la watu? Je, wana uwezo wa kutubu? Wao hupeperusha bendera ya imani, wakitekeleza shughuli za binadamu, wakitekeleza usimamizi wao wenyewe, na wanakwenda kinyume na mpango wa Mungu wa usimamizi kwa ajili ya wokovu wa wanadamu. Matokeo yao ya mwisho ni kuchukiwa na kukataliwa na Mungu; Mungu hawezi kamwe kuwaokoa watu hawa, hawawezi kamwe kutubu, tayari wamekamatwa na Shetani—wamo mikononi mwa Shetani kabisa. … ikiwa watu hawawezi kufuata njia ya Mungu na hawawezi kuitembea njia ya wokovu, matokeo yao ya mwisho yatakuwa yapi? Matokeo yao ya mwisho yatakuwa sawa na wale wanaoamini Ukristo na Uyahudi; hakutakuwa na tofauti. Hii ni tabia ya Mungu ya haki! Bila kujali umeyasikia mahubiri mangapi, na umeelewa ukweli kiasi gani, ikiwa hatimaye bado unawafuata watu na kumfuata Shetani, na hatimaye, bado huwezi kufuata njia ya Mungu na huwezi kumcha Mungu na kuepukana na uovu, basi watu kama hawa watachukiwa na kukataliwa na Mungu. Kadiri ionekanavyo, watu hawa ambao wanachukiwa na kukataliwa na Mungu wanaweza kuzungumza mengi kuhusu maandiko na mafundisho, na ilhali bado hawawezi kumwabudu Mungu; hawawezi kumcha Mungu na kuepukana na uovu, na hawawezi kuwa na utiifu mkamilifu kwa Mungu. Machoni pa Mungu, Mungu anawafafanua kama dini, kama kikundi tu cha wanadamu, na kama makao ya Shetani. Wanajulikana kwa jumla kama kikundi cha Shetani, na wanadharauliwa kabisa na Mungu.
kutoka katika “Ukiiishi mbele ya Mungu Kila Wakati tu Ndio Unaweza Kuitembea Njia ya Wokovu” katika Kumbukumbu za Maongezi ya Kristo
Madondoo ya Mahubiri na Ushirika kwa ajili ya Marejeo:
Tunamaanisha nini tunapoongea kuhusu “kumfuata Mungu”? Tunaongea kuhusu kupitia kazi ya Mungu na kukubali ukweli. Iwapo hukubali ukweli, iwapo hupitii kazi ya Mungu, basi hutapitia hukumu na adabu ya Mungu, ambayo inamaanisha humfuati Mungu. Je, tunawaita vipi wale ambao hawamfuati Mungu lakini ambao humwamini Mungu? Tunawaita waumini wa dini. Je, imani ya aina hii ya wale wanaomwamini Mungu haiko ndani ya dunia ya dini? Wanamwamini Mungu aliye mbinguni pekee, lakini hawamfuati Mungu, hawapitii kazi ya Mungu, wanashikilia tu Biblia yao, wanashikilia tu wanaloita andiko. Kila siku, wanasoma aya na kusali kwa njia ya dini, na inakoma hapo. Haina uhusiano wowote na maisha yao wenyewe, na jinsi wanavyoishi. Wanafanya tu chochote wanachofikiri wanapaswa kukifanya. Hii ndiyo inajulikana kama kuwa muumini wa dini. Hawakubali kazi ya Mungu, wala hawapitii kazi ya Mungu. Kwa hivyo, imani yao iko hapo tu kujaza uwazi ulioko katika roho zao, kuridhisha mioyo yao inayoteseka, na kutafuta aina fulani ya riziki. Je, watu wenye imani kama hii wataweza kuwa na ushuhuda mkubwa, mzuri kwa Mungu? Hakika hawataongea kuhusu kuwa na ushuhuda, kwa sababu hawajadili gharama, wala matumizi, wala utiifu, wala uzima. Kwa sababu ya hili, hawashuhudii. Kwa hivyo, wakati wowote wanapoteswa, kuna wachache sana kati yao ambao wanaweza kusimama imara. Wakati maisha yao yako hatarini, wote wanamsaliti Mungu. Pengine wengine wenu mtakanusha kile ambacho nimesema karibuni, pengine mtaniambia: “Katika Enzi ya Neema na katika Enzi ya Sheria, je, hakukuwa na mashahidi wengi?” Hilo si makosa. Hao mashahidi walikuwa na kazi ya Roho Mtakatifu, wao pia walikuwa wafuasi wa Mungu katika enzi hizo, kama tu tulivyo leo. Hawakuwa sehemu ya waumini wa dini. Wale waliopitia kazi ya Mungu katika Enzi ya Sheria walikuwa watu waliomfuata Mungu katika Enzi ya Sheria. Wale waliopitia kazi ya Mungu katika Enzi ya Neema walikuwa watu waliomfuata Mungu katika Enzi ya Neema. Katika Enzi ya Ufalme, wale kati yetu ambao hupitia kazi ya Mungu katika siku za mwisho pia ni wafuasi wa Mungu. Hata hivyo, sasa Mungu mwenye mwili wa siku za mwisho akitekeleza kazi Yake binafsi, kwa waumini ambao bado wako katika Enzi ya Neema na wale katika Enzi ya Sheria, imani zao zimegeuka kuwa imani za dini.
kutoka katika “Majadiliano Mengine Kuhusu Umuhimu na Maana ya Kutafuta Ukweli” katika Mahubiri na Ushirika Kuhusu Kuingia Katika Maisha XI
Kwanza, lazima tuelewe jinsi ambavyo jamii za kidini zilivyoundwa na tofauti kati ya kanisa na dini. Ni muhimu sana kuyafafanua masuala haya. Tunaona kutoka kwenye Biblia kwamba wakati wa kila hatua ya kazi ya Mungu, watu wateule wa Mungu waliongozwa na kuchungwa na wale ambao Mungu mwenyewe aliwaweka na kuwateua. Kwa mfano, wakati wa Enzi ya Sheria, Mungu alimtumia Musa kuwaongoza moja kwa moja watu wa Israeli, na Akamfanya Musa aunde mfumo wa kikuhani. Baada ya kazi ya Musa kukamilika hakukuwa na watu zaidi duniani ambao waliteuliwa moja kwa moja na Mungu kuwaongoza Waisraeli. Makuhani wakaanza kuchaguliwa na watu. Huu ni usuli wa uundaji wa jamii ya kidini ya dini ya Kiyahudi. Kuanzia hapo, mfumo wa kikuhani katika Uyahudi umekuwa ukiundwa kwa chaguzi kutoka katika jamii za kidini. Mara nyingi zaidi, jamii za kidini zilizidi kuwa potovu hatua kwa hatua kwa sababu makuhani ambao si sahihi walichaguliwa. Wakati ambapo Bwana Yesu mwenye mwili alionekana na kufanya kazi wakati wa Enzi ya Neema, jamii za kidini zilikuwa zimeanguka kwa kiwango kwamba zilipinga na kumlaani Kristo na kuwa maadui wa Mungu. Huu ni ukweli ambao kila mtu wakati huo aliweza kushuhudia. Bwana Yesu alipokuja duniani kufanya kazi Yake ya ukombozi, Yeye binafsi aliwachagua mitume kumi na wawili. Roho Mtakatifu pia alianza kufanya kazi wakati ule, na alikuwa pamoja na mitume wa Bwana Yesu. Katika wakati huu kusanyiko la wale waliokuwepo duniani ambao waliikubali kazi ya Bwana Yesu waliitwa kanisa, na walichungwa kikamilifu na watu walioteuliwa na Mungu, kwa maneno mengine, watu waliotumiwa na Roho Mtakatifu. Katika wakati huu, kanisa la kweli liliundwa, na hiki ndicho chanzo cha kanisa. Zaidi ya miaka thelathini baada ya kufufuka na kupaa kwa Bwana Yesu kwenda mbinguni, wengi wa mitume kumi na wawili walikuwa wamekufa kwa ajili ya imani, na kanisa duniani halikuchungwa tena na mitume waliokuwa wameteuliwa moja kwa moja na Bwana Yesu. Kwa hiyo, aina mbalimbali za vikundi vya kidini viliundwa. Huu ndio usuli wa uundwaji wa jamii za kidini wakati wa Enzi ya Neema. Baada ya hapo, bila kujali iwapo watu walikuwa na kazi ya Roho Mtakatifu au la, ilimradi waliweza kuzungumza kuhusu Biblia, wangeweza kuliongoza kanisa. Ilimradi walikuwa na karama, watu wangekubaliana nao na kuwafuata. Wangeweza kufanya kazi na kuhubiri kama walivyopenda bila mtu yeyote kuwazuia, hivyo madhebebu mbalimbali yalianza kuundwa. Kanisa ni nini, na dini ni nini? Tunaweza kusema kwamba makundi yanayoongozwa na kuchungwa na watu wanaotumiwa na Roho Mtakatifu ni makanisa, huku yale yanayoongozwa na kuchungwa na watu ambao hawatumiwi na Roho Mtakatifu ni dini. Huu ndio mgawanyiko rahisi kabisa na wa kweli kabisa. Makanisa ya kweli yana kazi ya Roho Mtakatifu Kazi ya Roho Mtakatifu kwa nadra sana huonekana katika dini, na hata ikionekana, ipo tu katika watu wachache ambao kweli wanamwamini Mungu na wanafuatilia ukweli. Hii ndiyo tofauti kati ya kanisa na dini. Kwa makanisa, ni jambo la muhimu sana kama wachungaji wanashughulikiwa na kutumiwa na Roho Mtakatifu au la. Ikiwa mchugaji ni mtu ambaye anafuatilia ukweli na anatembea kwenye njia sahihi, basi kazi ya Roho Mtakatifu ipo. Ikiwa mchugaji si mtu ambaye anafuatilia ukweli na anatembea kwenye njia ya Mafarisayo, basi kazi ya Roho Mtakatifu haipo. Ilimradi watu wanaweza kutofautisha kati ya wachugaji wa kweli na wa uongo, basi wanaweza kulipata kanisa la kweli.
kutoka katika “Kwa nini Ulimwengu wa Dini Umekataa Mungu Daima Huku Ukimtumikia” katika Mkusanyiko wa Mahubiri—Ruzuku ya Maisha
Views: 129 | Added by: flickrpinquorettfb | Tags: Ukweli Zaidi wa Injili, maisha ya kanisa | Rating: 0.0/0
Total comments: 0
avatar